Wednesday, March 30, 2011

Bado vikombe zaidi vinakuja!

Kilianza kikombe cha Babu kule Loliondo (KKKT)….kisha kikombe cha brazameni kule Rombo (Mkatoliki); Bibi kule Tabora (Mkatoliki) na kule Mbeya Babu dogo (yawezekana akawa mMoravian huyu …lol).

 

Tutarajie sasa Waislam, Wasabato na Waanglikana nao kuja na vikombe vyao…andaeni makoo yenu kupitisha hayo madawa!

Monday, March 21, 2011

Hakuna haja ya kuwa na Katiba Mpya!

Kuwa na viongozi wa aina ya Pinda Mizengo ambaye anamzuia Magufuli kutekeleza kazi yake kunanifanya nisione haja ya kuwa na katiba mpya.

 

Kuwa na viongozi wa aina ya Wasira Tyson mwenye mawazo ya kuwa serikali itakosa uvumilivu kutokana na maandamano ya CHADEMA wakati serikali hiyo hiyo inakuwa na uvumilivu kwa mafisadi na wakoloni wanaotorosha rasilimali zetu kunanifanya nisiwe na shauku ya kuwa na katiba mpya!

 

Kuwa na viongozi wa aina ya JK wanaolalamika tuuu bila kuchukua hatua na kuchochea visivyokuwepo kunanifanya nisione haja ya kuwa na Katiba mpya.

 

 

Aaaaargh, nilikuwa naota! naihitaji katiba mpya itakayoondoa uwezekano wa kuwa na viongozi wa namna hiyo!

Thursday, March 17, 2011

Ujinga unazidi…Elimu ya ngumbaru irejee!

Bila shaka utakubaliana nami kuwa kiwangi cha ujinga katika nchi yetu kimeongezeka. Natamani enzi zile za elimu wa watu wazima almaarufu ngumbaru irejeshwe tena katika kasi yake ile ile iliyokuwepo enzi za Mwalimu.

 

 

Enzi hizo kule Usukumani kwa akina Prof. Masangu Matondo kulikuwa na wakati wenyewe wanatoa vioja vinavyosaidia kukumbuka walojifunza.

 

 

Kwa mfano:

Sisi sote ni ndugu wao walisema jiji soda mundugu  yaani hizi soda kwenye ukuta

 

Tukuyu, Pemba na Maswa wao walisema duguyu pemba na maswa wakimaanisha tutakuwa tunawasha na majani!

 

Kuna wimbo: Naapa naahidi mbele ya chama mapinduzi nitayalinda mpaka kufa wao waliimba Napanda mbiti yale-ha chama yupinduka unayunilola mpaka yucha wakimaanisha nimekanyaga fisi ilikuwa ya chama ikageuka ikaniangalia mpaka ikafa!

 

Kwa burudani hiyo ya maneno wao waliweza kukumbuka waliojifunza japo ki-komedi! Natamani kuingia darasa la ngumbaru nikafundishe japo kuna changamoto.

Monday, March 14, 2011

Tatizo si Tanesco ama TRC

Kwa muda sasa watu wa kawaida wakiwemo wanasiasa wamekuwa wakitoa zigo la lawama kwa TANESCO, ATCL, TRC ama TAZARA kwa utendaji wao mbovu.

 

Hata hivyo watawala wetu manyang’au ndio wa kulaumiwa kwa uozo huu kwani kwa makusudi mazima wamedhoofisha mashirika hayo ili kujitengenezea ulaji. Hivyo inashangaza sana wanasiasa wanapolaumu mashirika hayo kwa utendaji wao ilhali kwa namna moja ama nyingine wana mkono wa dhuluma dhidi ya wananchi wa nchi hii.

 

Umeme: Tunao wataalamu ambao wamesomeshwa na Mzee wa Mwitongo katika nyanja za ‘geothermal’,  wind na ‘solar’ na kubobea katika fani hizo. Ikumbukwe maji moto (geothermal) yanapatikana ktk ukanda wa bonde la ufa (rift valley); upepo tunao mwingi tu wa kutosha na jua ni la kumwaga bila chenga! Huko Songwe kwa mfano kiwango cha geothermal kilichopo kinaweza kuzalisha 300mW! Wataalamu wetu hawa wamebaki kungoja kuhudhuria semina, warsha na mikutano ya kimataifa ilhali walichokisomea kipo. Bonde la Stigler gorge linaweza k,uzalisha zaidi ya 2000mW lakini plani ya mzee mchonga ilichakachuliwa na wakubwa wakaamua kujenga Kihansi.

 

TAZARA, ATCL, na TRC: kama ilivyo kwa umeme uchakachuaji wa mashirika hayo pia umedhoofisha utendaji wake. Wakubwa siku zote wamekuwa wakiingilia utendaji wao ili wao waweze kunufaika.

 

Ili wakubwa waweze kunufaika wameamua kung’ang’ania juu ya majenereta ya kuzalisha umeme kwani huko ndo kwenye dili. Hali kadhalika tumeshuhudia ongezeko la mabasi ya kwenda mikoa ilokuwa ikihudumiwa na reli na ndege. Mabasi hayo pamoja na malori ya mizigo yanamilikiwa na wakubwa wetu! Mbunge mmoja wa huko Rukwa kwa mfano ameingiza magari makubwa matano (semi-trailers) kwa ajili ya usafirishaji wa mizigo.

 

Hivyo tunapojadili upandaji wa gharama na hali  ngumu ya maisha wanasiasa/watawala wanaosingizia kupanda kwa MAFUTA ni UJINGA na WIZI mtupu!