Thursday, October 28, 2010

Nawatakia Uchaguzi mwema!

Nimekuwa mtoro sana kijiweni hapa. Niko likizo lakini ni kama niko job tu kwa kuwa ninaandaa maadhimisho ya siku ya Wavuvi Duniani ambayo itafanyika Musoma. Maadhimisho hayo yatafanyika kikanda (Afrika Mashariki) ambapo kutakuwa na washiriki (wavuvi) kutoka Rwanda, Burundi, Kenya, Tanzania na Uganda!

Ukiongeza hekaheka za uchaguzi ndo kabsaaaaa!

Kwa wale watakaopiga kura nawatakia upigaji kura mwema na tutaonana huko kwani nitakuwa mmojawapo wa waangalizi wa ndani wa uchaguzi (iwapo hakutakuwa na mizengwe).

Kwa wale ambao hamtapiga kura kwa sababu moja ama nyingine, mtiombee zoezi hili liende mswano.

Saturday, October 23, 2010

Undumilakuwili utatumaliza wazima wazima!

Photo-0012 Gari aina ya fuso

 

Wakati tunaelekea mwishoni mwa kampeni tayari kuna dosari imeshajitokeza kwenye uongozi na dira kama taifa. Dosari hii kwa maoni, mtizamo wangu ni kuwa chama changu tawala hakistahili tena na kamwe kupewa ridhaa ya kuongoza nchi hii tukufu.

 

Kuna tuhuma zilitolewa na mmojawapo wa wagombea kuwa chama kimoja cha siasa kinatumia genge la vijana wanaojishughulisha kufanya vitendo vya uhalifu hapa mjini Musoma. Vikundi hivyo ni Jamaica Mockers na Mbio za Vijiti. Ilidaiwa kuwa vinana hao wanasafirishwa na gari aina ya fuso (pichani) na wana mapanga na mijeledi pamwe na silaha nyingine za jadi kwa ajili ya ‘kuwashughulikia’ vyama pinzani!

 

Taarifa zilizopo ni kuwa polisi walilikamata gari hilo likiwa na silaha hizo lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa. Tukumbuke kuwa vikundi hivi vya vijana ndivyo vinahusika na vitendo vibaya vya ubakaji na uporaji. Siku ya mwisho ya mtihani wa kidato cha nne, mmojawapo wa wanachama wa Jamaica Mockers aliyekuwa anasoma kidato cha nne katika shule ua Musoma Utalii Sec alikamatwa kwa ubakaji wa msichana wa kidato cha kwanza wa shule hiyo.

 

Tatizo langu ni kuwa: kwa nini chama cha siasa kijihusishe na makundi haya ya kishenzi ilhali mkuu wa kaya ambaye ni mkuu wake akijinadi kuwa wametokomeza ujambazi na kuwa vibaka hakuna na kwamba hali ya usalama/amani ni nzuri? Inatia uchungu kuona hayo yakitendeka wakati huu na yakiwahusisha vijana ambao wanatumiwa vibaya-badala ya kuwafanya wawe raia bora wanawafanya baadae wawe maadui wao wenyewe na jamii.

 

Ikumbukwe kuwa hatuna sera nzuri ya vijana na mara zote vijana wamekuwa wakitumika kuwaingiza wanasiasa madarakani na kisha kuwabwagilia mbali. Kwa mfano kwenye mabilioni ya JK tumeshuhudia vijana wakikosa mikopo ilhali watu wazito wakiipata kwa kutumia mashamba hewa! Kiukweli vijana wanakuwa ‘watamu’ wakati wa uchaguzi na unapoisha wanakuwa maadui baada ya uchaguzi!!

 

Nitashangaa sana baada ya uchaguzi kama polisi watajidai kuwasaka wanachama wa vikundi hivi hasa wakati wakubwa wanazuru mkoa wakati walikuwa hawachukui hatua yoyote wakati huu!

 

Aaagh!

Tuesday, October 19, 2010

Wengi wetu ni Mawenzi na wachache wetu ni Kibo, ama!

 192516-largest_29344

Bila shaka mnakumbuka kisa cha Kibo na Mawenzi katika simulizi za hadithi katika shule ya msingi ambapo Kibo na Mawenzi walikosana kwa sababu ya wivu na uvivu wa Mawenzi akamwagia kaka yake Kibo uji wa moto kichwani (theluji kama inavoonekana sasa) na Mawenzi kuishia kupigwa kwa mwiko kichwani mpaka akawa nyang’anyang’a.

Wivu na uvivu, hulka ya Mawenzi ilimfanya akabwengwa na kaka yake Kibo katika ugomvi uloanzishwa na Mawenzi. Bidii ya kazi na utendaji wa kujituma ilimfanya Kibo akamwagiwa uji wa moto kichwani! Kibo anapendeza (uji a.k.a theluji) kutokana na bidii na Mawenzi ni mbofumbofu kutokana na wivu na uvivu!! Aaagh! Si unaona wanaofanya kazi wanavyobezwa na mafisadi wanavyotukuzwa?

Majuzi mkubwa wa kaya akimnadi mtu mmoja huko Rombo akasema ati wamchaguwe mtu huyo kwa kuwa kakesi aliko nako ni kadogo sana na kuwa mkuu wa kaya ana hakika ntu huyo atashinda! Nikadhani ni masikhara nkastukia na Monduli nako anamnadi mtu kuwa ni msafi saaana kama sufi, mh! Nasubiria Igunga nisikie tena stori!

Viongozi na wazee wetu sijui wanatupeleka wapi ama siye ndo tunajipeleka kusiko!

Friday, October 15, 2010

Taswira za kuadhimisha miaka 11 ya kifo cha Mwl. Kambarage Nyerere!

 

Photo-0021(01)

Baba Askofu Michael Msonganzila wa jimbo Katoliki la Musoma akiendesha misa ya kumbukizi la miaka 11 ya kifo cha Mwl. J.K. Nyerere iliyofanyika jana huko Butiama. Katika homilia yake Askofu Msonganzila alizungumzia wasifu wa Baba wa Taifa mintaarafu uchaguzi ujao. Mambo kama ustawi wa watu, amani, heshima na haki kwa wote vilitawala maisha ya Mwalimu. Mambo muhimu aliyosema:

“pengo kati ya walionacho na wasiokuwa nacho linaongezeka. Kadiri linavyoongezeka ndivyo na wasiokuwa nacho wanavyo jawa na hasira kwa kuwa wanafalsafa wanasema kuwa mtu mwenye njaa huwa na hasira na siku zote hasira itajitokeza nje kwa namna mbalimbali”

 

“Mwalimu aliwaweka watu kama hatma ya kila jambo alilokuwa analifanya ktk nchi hii maendeleo ya watu) tofauti na viongozi wa sasa wanawatumia watu kama nyenzo/vyombo vya kutekeleza matakwa/tamaa zao mbaya kisiasa”

 

“rushwa na maovu mengine yanatamalaki katika jamii yetu kwa kuwa kuna tamaa mbaya za aina mbalimbali. Kwa bahati mbaya viongozi wa dini wakiyazungumzia wanaambiwa wavue majoho waingie kwenye siasa. mbona tukifanya kazi za jamii kama kujenga hospitali na mashule tunasifiwa, kwa nini katika hili la kukemea maovu tuambiwe tukavue majoho tufanye siasa”

 

“mchakato wa kumtangaza Mwalimu kuwa Mtakatifu uachwe utendeke kwa mujibu wa kanuni na taratibu za kanisa katoliki na usiingiliwe kwa namna yoyote ile ili uamuzi utakapotolewa uwe ule ambao unathibitishwa bila shaka yoyote”

Photo-0022(01)

Umati wa watu ukiwa kaburini mara baada ya misa kwa sala na maombi.

Photo-0023(01)

Watu wakijumuika Mwitongo.

14102010015

 

Kundi la baadhi ya wana maombi kutoka Dar Es Salaam wakiongozwa na Pd Felician Nkwera na Sr. Dina nao walikuwa miongoni mwa wageni waliofika kwa ajili ya kuungana na Mama Maria Nyerere na familia yake ktk mkesha na misa ya kumbukumbu hiyo.

Wednesday, October 13, 2010

Hongera kwa siku yako ya kuzaliwa!

IMG0015AJack Ng’wanaMayenga! 

 

Ati leo tarehe 14 Oktoba umezaliwa upya! Hongera Da Jack Ng’wana Mayenga kwa kutimiza miaka kadhaaa. Ujaaliwe miaka mingi na kheri duniani. Uwalee wanao Nyamtondo na Nkugi katika maadili ya kisukuma haswaaaa!

 

Hongela! Unibakishie keki ya viazi!

Thursday, October 7, 2010

Lugha zetu zinapotea: Nani mchawi?

nyankole  Binti wa kinyankole!

 

Kwa siku kadhaa tumekuwa hapa Machame tukizungumzia juu ya mchango wa mila na tamaduni katika utunzaji na usimamizi wa mazingira. Mojawapo ya changamoto ambazo wazee tulokuwa nao wameziongea ni upoteaji wa lugha.

 

Si ajabu Da Yasinta alipoanzisha blog ya kilugha baadhi ya watu walimshangaa. Kwa hiyo wazee wanasema kuwa vijana wa sasa hawajui kabisa lugha zao na wametekwa na utandawazi-wizi….kwamba kuongea Kiswahili sana na kimombo ndo unaonekana wewe ni wa maana mno!

 

Mama (mzee) mmoja wa kichaga alisema kwa sasa ni vigumu kwa wazee kuwasiliana na watoto hasa kwa masuala ya msingi ambayo mtu asiyehusika hatakiwi kujua ni ngumu. Kwa mfano kama binti alikaa vibaya mbele za watu aliambiwa KAANISHA kwa Kichagga ama kwa binti wa Kinyankole (kabila la kusini mwa Uganda) aliambiwa SHITAMAJI na moja kwa moja alielewa nini kinaongelewa na hivyo kujikusanya na kukaa kwa adabu na staha zaidi.

 

Lakini sasa watoto wameota mapembe hawataki kusikia ya mwadhini wala ya mnadi swala!  Ukimuongelesha kilugha anadai mzazi amepitwa na wakati na hata kuongea wenyewe kwa wenyewe wanambiana ama kuambiwa kuwa ni WAPORIPORI yaaani washamba!

 

Nani mchawi? Elimu, watoto ama Wazee?

Ukiona UMEULA jua USHALIWA!

ugimbi Jamaa wakipata ugimbi kwa raha zao!

 

Juzi mke wa rafiki yangu karejea saa mbaya (usiku wa manane) akiwa na chupa kadhaa za ulabu akimletea mumewe naye agide!

 

Rafiki yangu anasema kuwa mgombea ubunge mmoja hapa jimboni Musoma mjini alitoa ofa ya kufa mtu katika kitongoji cha Rwamlimi na watu walijitwalia kiasi wanachotaka!

 

Nilipomuuliza rafiki yangu juu ya msimamo wake wa kutoa kura akadai kuwa atatoa kwa mtoa ofa ya ulabu! Nimecheka sana huku nikiwa namshangaa kwa kuwa ni huyo huyo ambaye kila nikikutana naye ananambia kuwa maisha ni magumu na kuna haja ya kufanya mabadiliko!

 

Inaonekana haelewi kuwa UKIONA UMEULA ujue UMELIWA!!!!!!! Kalagabaho…!

Tuesday, October 5, 2010

Hivi, huwezi kutoa huduma mpaka upewe hongo?

Photo-0022

Mizigo ikiwa imetolewa nje ya nyumba!

Nimeanza likizo lakini kwa kichefuchefu! Kichefuchefu hiki kinatokana na niliyoyakuta kijijini siku ya kwanza ya likizo yangu. Nilipofika huko nilikuta zoezi la umwagiliaji dawa ya kuua mbu ndani ya nyumba (indooor residue spray) likiendelea. Na nilifurahi walau kuona watu wakitoa vyombo japo kuna baadhi walikuwa wanagoma dawa kunyunyizwa ndani ya nyumba zao.

Photo-0023

Mmwagiliaji akiwa kazini katika kituo cha Madaraka, kata ya Kukirango.

 

Kilichonitia kichefuchefu ni taarifa za kuwepo vitendo vya hongo kwa hao waliohusika na zoezi la unyunyiziaji wa dawa.  Kutoka wilayani Bunda nimepata nakala ya barua ya mwananchi mmoja ambaye aliandika kwa Takukuru, DC, DMO, DED nk akilalamikia jinsi zoezi la usaili wa watu watakaohusika na unyunyizaji lilivyokwenda.

 

Mtu wa Bunda alisema ili kupata fomu ya kuomba kazi hiyo ilikupasa utoe sh. 6,000 na ukiitwa kwenye usaili unalipa sh. 50,000 ambazo hazitarejeshwa.

 

Musoma vijijini baadhi ya wanaohusika kwenye zoezi hilo wanadai kuwa kuna baadhi wametoa hongo mpka ya sh 200,000 kwa kila mmoja.

 

Jamani, hivi kutoa huduma mpaka mtu atoe hongo?

Saturday, October 2, 2010

Wikiendi njema kwa vimbwanga toka kwa mdau FeDE na wengineo!

 

Ed JK KE Katiba

Mambo yako hivo?!!!!

Ed JK Ambulance 

Kasheshe hilooo!

kwa wababa

Haya kwa mwenye kuitaji usaidizi….lol!

Friday, October 1, 2010

Ujuzi wa mila na desturi na kuongezeka kwa uweledi wa wanafunzi katika somo la historia!

 localhut

Mtoto akiwa langoni mwa nyumba! 

 

Niko Machame na nimetembelea shule tatu za msingi zilizoko katika kata ya Machame Kaskazini. Shule hizo ni Nkweseko (1937), Nkwawangya (1975) na Nkwamwasi (1962). Shule hizo kwa pamoja zimejenga nyumba za asili za kichaga na kuziwekea vifaa (artifacts) vya zamani vilivotumika kwa maisha ya kawaida ya wachaga. Vifaa hivo vinakusanywa na watoto wenyewe toka majumbani mwao.

 

Nyumba hizo sasa zinatumika kama vituo vya mafunzo kwa wanafunzi na jamii ambapo wazee na wanafunzi hukutana na kuelezana mila na desturi za kichaga. Humo utakuta vitu kama kidewa (chombo kama bakuli kilichotengenezwa kwa mti kilichotumika kwa kulia chakula) nk. Wazee hufundisha watoto mambo ya zamani…mila na desturi za kichaga, walipotoka, jinsi walivoishi, vita walivyopigana kujikomboa na maadui zao nk!

 

Ni hapa nilipokutana na simulizi toka kwa mtoto akinambia zamani nyumba za wachaga wa machame zilipojengwa milango haikutazama kibosho kwa kuwa kulikuwa na uadui wa jadi uliotokana na mapigano ya mara kwa mara. Hata kuoana haikuwa rahisi. Na akanambia kuwa hilo sasa ni kama limekwisha kutokana na ujio wa dini na pia watu kustaarabika!

Kwa maelezo ya walimu wakuu wa shule hizo kiwango cha uelewa cha wanafunzi katika somo la historia kimepanda. Pengine wana vigezo vyao lakini kwa mazungumzo na wanafunzi wachache walionekana kufurahia hilo jambo. Walimu na wanafunzi wanakiri kuwa uwezo wa kitaaluma ktk somo la historia umepanda na pia sayansi.

 

Nadhani kuwa na mbinu kama hii ya kufundishia (kuwa na nyumba za jadi-mahalia) ni jambo jema kujifunza, ne?